JW subtitle extractor

“Yehova Aliwafanya Washangilie”

Video Other languages Share text Share link Show times

“Mtumikieni Yehova kwa kushangilia,”
inasema Zaburi ya 100:2.
Naam Yehova anataka
tuwe wenye shangwe.
Naye ametupa sababu
nyingi za kushangilia.
Alitupatia uhai
ambao una sababu nyingi
zinazotufanya tuwe na shangwe.
Alitupatia Biblia
inayotufundisha
jinsi ya kufurahia maisha.
Na anatuelekeza kwa njia nyingi
zinazotuletea shangwe.
Kweli, Yehova ni Mungu
anayewapa watu shangwe.
Hata hivyo,
Shetani hataki tupate
shangwe kwa kumtumikia Yehova.
Kwa nini?
Kwa sababu, kwanza
anajua shangwe inatusaidia
kuendelea kuhubiri na kufundisha
na hiyo ndiyo kazi
anayotaka kukomesha.
Kwa hiyo, anajaribu
kuharibu shangwe yetu,
iwe ni kupitia marufuku
kutoka kwa serikali
au upinzani kutoka kwa familia
au jamii yetu.
Pia Shetani anataka
tupunguze utumishi wetu
kwa Yehova ili kutafuta
vitu vya kimwili
ambavyo si vya lazima.
Anataka tufikiri kwamba
kupata vitu vingi zaidi vya kimwili
kutatuletea shangwe ya kudumu.
Lakini haviwezi kutuletea shangwe.
Mbinu hizo za Shetani si mpya.
Tutakaposoma sehemu za
vitabu vya Ezra,
Hagai,
na Zekaria,
tafuta masomo
yanayoweza kutusaidia
‘kumtumikia Yehova
kwa kushangilia’ leo.
Jaribu kutafuta
ni mambo gani yaliyowaletea
watu wa Yehova shangwe,
na ni mambo gani
yaliyowanyima shangwe.
Na ufikirie ni kwa nini
tunaweza kupata
“shangwe ya Yehova” leo,
na jinsi ya kuipata,
hata chini ya hali ngumu.
Ezra,
kuhani na mwandishi wa
Sheria ya Musa,
ndiye aliyeandika kitabu
kinachoitwa kwa jina lake.
Ambacho kinaendelea
kuzungumzia historia ya taifa la Israeli
baada ya matukio
tunayosoma kwenye Mambo ya
Nyakati cha pili.
Huenda Ezra
ndiye aliyeandika kitabu hicho.
Ni mwaka wa 537 K.W.K.,
na Wayahudi wengi wako
karibu kurudi Yuda.
Taifa hilo limekuwa utekwani
Babiloni kwa miaka 70
kwa sababu ya ibada ya sanamu.
Wamejifunza somo muhimu,
na hakuna wakati ambapo taifa lote
linarudia ibada ya sanamu tena.
Sasa wakati umefika
wa kurudisha ibada safi
Yerusalemu.
Simulizi hilo linazungumzia
mambo yaliyotokea wakati wa
wafalme kadhaa wa Uajemi,
kuanzia na Mfalme Koreshi,
na linaanza kwa matukio yenye shangwe.
Tafadhali fungua Ezra 1:1 hadi 6,
tusome pamoja.
Katika mwaka wa kwanza
wa utawala wa Mfalme Koreshi
wa Uajemi,
ili neno la Yehova
lililosemwa na Yeremia litimie,
Yehova aliichochea
roho ya Mfalme Koreshi wa Uajemi
atoe tangazo katika ufalme wake wote,
ambalo pia aliliandika,
akisema:
Mfalme Koreshi wa Uajemi anasema hivi:
‘Yehova Mungu wa mbinguni
amenipa falme zote za dunia,
naye ameniagiza nimjengee
nyumba Yerusalemu,
nchini Yuda.
Yeyote miongoni mwenu,
ninyi watu wake wote,
Mungu wake na awe pamoja naye,
na apande kwenda Yerusalemu,
kule Yuda,
na kuijenga upya
nyumba ya Yehova Mungu wa Israeli
yeye ndiye Mungu wa kweli
ambaye nyumba yake
ilikuwa Yerusalemu.
Na mkaaji mgeni yeyote,
popote alipo,
majirani zake wamsaidie
kwa kumpa fedha na dhahabu,
mali na wanyama wa kufugwa,
pamoja na toleo la hiari
kwa ajili ya nyumba ya Mungu wa kweli,
iliyokuwa Yerusalemu.”
Ndipo viongozi wa ukoo wa Yuda
na Benjamini
na makuhani
na Walawi
kila mmoja ambaye roho yake
ilichochewa na Mungu wa kweli
wakajitayarisha kupanda
kwenda kujenga upya nyumba ya Yehova,
iliyokuwa Yerusalemu.
Wale wote waliowazunguka
wakawasaidia kwa kuwapa
vyombo vya fedha
na dhahabu,
mali,
wanyama wa kufugwa,
na vitu vyenye thamani,
mbali na matoleo yote ya hiari.
Hebu wazia!
Yehova anawarudisha
Wayahudi katika nchi yao
wakiwa na agizo kutoka kwa
Mfalme Koreshi mwenyewe
la kujenga upya hekalu.
Wayahudi wengi wanakubali
kwa shangwe mgawo huo.
Hata hivyo,
wale ambao hawangeweza kurudi
wanatoa msaada wa kifedha
kwa wale ambao wangeweza.
Huenda mapema katika
masika ya 537 K.W.K.,
Waisraeli 50,000 hivi
wanaondoka Babiloni.
Wanaongozwa na kuhani mkuu
Yeshua,
ambaye pia anaitwa
Yoshua,
na gavana ambaye
Koreshi amemweka rasmi,
Zerubabeli.
Wanafika Yuda mapema
katika majira ya vuli,
nao wana shangwe!
Lakini wafanye nini
ili kudumisha shangwe yao?
Ona kile wanachofanya mara tu
wanapozoea mazingira yao mapya.
Tusome Ezra 3:1 hadi 6:
Mwezi wa saba ulipofika
Waisraeli walikuwa katika majiji yao;
wakakusanyika Yerusalemu
wakiwa na kusudi moja.
Yeshua mwana wa Yehosadaki
na makuhani wenzake
na Zerubabeli mwana wa Shealtieli
na ndugu zake wakasimama
na kujenga madhabahu ya
Mungu wa Israeli,
ili kutoa dhabihu za
kuteketezwa juu yake,
kama ilivyoandikwa
katika Sheria ya Musa,
mtu wa Mungu wa kweli.
Basi wakajenga madhabahu
mahali ilipokuwa zamani,
ingawa waliwaogopa watu wa nchi jirani,
nao wakaanza kumtolea Yehova
dhabihu za kuteketezwa juu yake,
asubuhi
na jioni.
Kisha wakafanya Sherehe ya Vibanda
kulingana na ilivyoandikwa,
na siku baada ya siku
walitoa idadi iliyohitajika ya
dhabihu za kuteketezwa.
Baadaye
walitoa dhabihu za kuteketezwa
zilizotolewa kwa ukawaida
na matoleo kwa ajili ya miezi mipya
na majira yote yaliyotakaswa
ya sherehe za Yehova,
na pia toleo la hiari
la kila mtu
aliyemtolea Yehova kwa kupenda.
Tangu siku ya kwanza ya mwezi wa saba,
walianza kumtolea Yehova
dhabihu za kuteketezwa,
ingawa bado msingi
wa hekalu la Yehova
haukuwa umewekwa.
Je, ulitambua kwamba
Wayahudi walirudisha ibada ya Yehova
“ingawa waliwaogopa
watu wa nchi jirani”?
Kwa sababu ya kutenda kwa ujasiri,
hiyo inakuwa pindi
yenye shangwe sana kwao.
Inakuwa tu kama Musa alivyosema
alipoliagiza taifa
lisherehekee Sherehe ya Vibanda:
“Nanyi mtakuwa na shangwe kwelikweli”!
Mwaka unaofuata,
wanaweka msingi wa hekalu
kwa ujasiri na kwa shangwe.
Acheni tusome kuhusu hilo
kwenye Ezra 3:10 hadi 13:
Wajenzi walipoweka
msingi wa hekalu la Yehova,
makuhani waliovaa mavazi rasmi,
wakiwa na tarumbeta,
na Walawi,
wana wa Asafu,
wakiwa na matoazi,
wakasimama ili kumsifu Yehova
kulingana na maagizo ya
Mfalme Daudi wa Israeli.
Nao wakaanza kuimba kwa kuitiki
wakimsifu na kumshukuru Yehova
“kwa maana yeye ni mwema;
upendo wake mshikamanifu
kwa Israeli unadumu milele.”
Kisha watu wote wakapaza sauti
wakimsifu Yehova kwa sababu
msingi wa nyumba ya Yehova
ulikuwa umewekwa.
Makuhani wengi,
Walawi,
na viongozi wa koo
wazee ambao walikuwa
wameona ile nyumba ya kwanza
wakalia kwa sauti
kubwa walipoona
msingi wa nyumba hii ukiwekwa,
na wengine wengi wakapaza
sauti yao yote kwa shangwe.
Hivyo watu hawakuweza kutofautisha
kati ya sauti ya kushangilia
na ya kulia,
kwa maana watu walikuwa wakipaza sauti
kubwa hivi kwamba sauti hiyo ikasikika
mbali sana.
Naam, baadhi ya wazee wa taifa hilo
hawawezi kuwazia jinsi ambavyo
hekalu hilo lingeweza kufanana
na hekalu la Sulemani.
Lakini kelele zenye shangwe za watu
wengine zinafunika vilio vyao.
Hata hivyo, watu wa maeneo
yanayowazunguka hawafurahii jambo hilo.
Badala yake wanafanya mipango ya
kuzima shangwe yao.
Acheni tuone wanafanya hivyo jinsi gani
kwenye Ezra sura 4:1 hadi 3:
Maadui wa Yuda na Benjamini waliposikia
kwamba watu waliorudi
kutoka uhamishoni walikuwa wakimjengea
hekalu Yehova Mungu wa Israeli,
mara moja wakamfikia Zerubabeli
na viongozi wa koo
na kuwaambia:
Acheni tujenge pamoja nanyi;
kwa maana,
sisi pia tunamwabudu Mungu wenu
na tumekuwa tukimtolea dhabihu
tangu siku za
Mfalme Esar-hadoni wa Ashuru,
aliyetuleta hapa.
Hata hivyo,
Zerubabeli na Yeshua
na viongozi wa koo za Israeli
wakawaambia:
Hamna haki ya kujenga
pamoja nasi nyumba ya Mungu wetu,
kwa maana sisi wenyewe
tutamjengea Yehova
Mungu wa Israeli,
kama alivyotuamuru Mfalme Koreshi,
mfalme wa Uajemi.
Zerubabeli anatambua kwamba maadui hawa
hawana nia ya kuwasaidia,
bali wanataka kuwadhuru.
Ombi lao la kusaidia linapokataliwa,
wanajaribu kuwazuia
Wayahudi wasijenge hekalu.
Ona jinsi wanavyofanya hivyo
tunaposoma mstari wa 4 hadi 7:
Ndipo watu wa mataifa jirani wakazidi
kuwavunja moyo watu wa Yuda
na kuwakatisha tamaa ili wasijenge.
Waliwakodi washauri ili
kuvuruga mipango yao ya kujenga,
siku zote za Mfalme Koreshi wa Uajemi
mpaka wakati wa utawala
wa Mfalme Dario wa Uajemi.
Mwanzoni mwa utawala wa Ahasuero,
waliandika mashtaka
dhidi ya wakaaji wa Yuda
na Yerusalemu.
Na katika siku za utawala wa
Mfalme Artashasta wa Uajemi,
Bishlamu,
Mithredathi,
Tabeeli,
na wenzake
walimwandikia Mfalme Artashasta;
wakaitafsiri barua hiyo katika Kiaramu,
na kuiandika kwa herufi za Kiaramu.
Acheni tusome barua ambayo Rehumu,
ofisa mkuu wa serikali,
na maadui wengine wa Waisraeli,
wanamwandikia mfalme.
Ona ni mashtaka gani ya
uwongo wanayotoa,
tunaposoma Ezra 4:11 hadi 16:
Hii ndiyo nakala ya barua waliyomtumia.
Kwa Mfalme Artashasta
kutoka kwa watumishi wako,
watu walio Ng’ambo ya Mto:
Sasa tungependa kumjulisha
mfalme kwamba Wayahudi
waliokuja huku kutoka kwako
wamefika Yerusalemu.
Wanajenga upya
lile jiji lenye uasi na uovu,
nao wanamalizia kujenga kuta
na kurekebisha misingi yake.
Sasa tungependa mfalme ajue kwamba
ikiwa jiji hili litajengwa upya
na kuta zake kukamilishwa,
hawatalipa kodi,
ushuru,
wala ada,
na jambo hilo litasababisha hasara
kwa hazina za wafalme.
Na kwa kuwa sisi hula
chumvi ya jumba la mfalme
na si vema kwetu kuona
masilahi ya mfalme yakiathiriwa,
ndiyo sababu tumetuma barua
ili kumjulisha mfalme jambo hilo,
ili uchunguzi ufanywe katika kitabu cha
kumbukumbu za mababu zako.
Ndipo utakapoona katika kitabu hicho
cha kumbukumbu kwamba
hili ni jiji lenye uasi,
linalowaletea hasara wafalme na mikoa,
na tangu zamani lilikuwa
na wachochezi wa uasi.
Ndiyo sababu jiji hili
liliangamizwa.
Tunakujulisha mfalme
kwamba jiji hili likijengwa upya
na kuta zake kukamilishwa,
hutaweza kutawala tena
eneo lililo Ng’ambo ya Mto.
Je, umewahi kusikia mashtaka
kama hayo ya uwongo?
Ni kama yale ambayo
maadui wetu hutusingizia leo:
“Hawalipi kodi.
Waipinga serikali.
Wao ni waasi
na wanawachochea watu kuwa waasi.
Hawawezi kudhibitiwa.”
Bila shaka, hayo ni mashtaka ya uwongo!
Mashtaka hayo yaliathiri kazi ya Waisraeli.
Mfalme aliamuru kazi ikomeshwe,
na kazi ya kujenga upya hekalu ikakoma.
Inasikitisha sana!
Mwanzoni Wayahudi waliporudi,
hawakuruhusu woga wa wanadamu
uwazuie kufanya kazi ya Yehova.
Lakini sasa waliruhusu uwoga uwazuie.
Leo, maadui wetu wameongeza
upinzani wao dhidi ya kazi ya Yehova.
Lakini, kulegeza msimamo
au kuacha kabisa utendaji wetu
hakuwezi kuleta shangwe
kunaleta huzuni tu.
Lakini kudumisha uaminifu
kunaleta shangwe,
hata tunapokabili upinzani mkali.
Hilo linawezekanaje?
Fikiria mfano halisi.
Wazia mama na binti yake
wakiwa wamezungukwa na
kundi kubwa la wanaume wanaofanya
fujo na kujaribu kuwalazimisha kununua
kadi za chama cha kisiasa.
Akina dada hao watafanya nini?
Wakilegeza msimamo
na kununua kadi hizo,
maadui wao watafurahi.
Lakini ikiwa wangefanya hivyo
dada hao wangejisikia vibaya sana
baadaye kwa sababu
wanajua walimkana Baba yao wa mbinguni.
Dada hao hawakukubali.
Bila shaka, hawakufurahia
kudhihakiwa na kutendewa vibaya.
Hata hivyo, baadaye
dhamiri zao zilikuwa safi.
Na walikuwa na shangwe moyoni,
kwa sababu walijua walidumisha
uaminifu wao kwa Yehova.
Namna gani Wayahudi katika siku za Ezra?
Huenda wengi
waliacha maisha yenye starehe
Babiloni ili kufunga safari ndefu
na ngumu kurudi Yuda.
Sasa, baada ya miaka 14
ya kukabili upinzani,
kuanzia walipoweka msingi wa hekalu
hadi walipopigwa marufuku,
Wayahudi wamepoteza bidii yao
kwa ajili ya kazi ya Yehova.
Wanatoa dhabihu kidesturi tu,
lakini hawafanyi kile ambacho Yehova
aliwaagiza wafanye,
yaani, wamalize kujenga hekalu!
Wanapokabili upinzani,
wanafikia mkataa
kwamba huenda huu si
wakati wa Yehova wa
kukamilisha kazi hiyo.
Inaonekana kwamba hata
Gavana Zerubabeli na
kuhani mkuu Yeshua
wanahitaji kutiwa moyo.
Ili kuwatia moyo,
Yehova anamtuma nabii Hagai.
Sasa tufungue kitabu cha Hagai sura ya 1.
Ujumbe mzito na ulio wazi wa Hagai,
uliotolewa katika
kipindi cha miezi minne hivi,
unaonyesha wazi tatizo lilikuwa nini,
kama tunavyosoma
kwenye Hagai 1:2 hadi 11:
Yehova wa majeshi anasema hivi:
“Watu hawa wanasema,
‘Wakati wa kujenga nyumba ya Yehova
bado haujafika.’”
Na neno la Yehova likaja tena
kupitia nabii Hagai, likisema:
“Je, ni wakati wa ninyi kukaa
katika nyumba zilizopambwa kwa mbao,
huku nyumba hii ikiwa magofu?
Sasa hivi ndivyo anavyosema
Yehova wa majeshi,
‘Kazieni mioyo yenu juu ya njia zenu.
Mmepanda mbegu nyingi,
lakini mnavuna kidogo.
Mnakula,
lakini hamshibi.
Mnakunywa,
lakini hamtosheki.
Mnavaa nguo,
lakini hakuna yeyote anayepata joto.
Kibarua huweka mshahara wake katika
mfuko uliojaa mashimo.’
Yehova wa majeshi anasema hivi:
‘Kazieni mioyo yenu juu ya njia zenu.
Pandeni juu mlimani mkalete miti.
Jengeni nyumba hii,
ili niifurahie
na ili nitukuzwe,’
asema Yehova.
‘Mlitazamia mavuno mengi
lakini mlipata kidogo;
na mlipoyaleta katika nyumba hii,
niliyapeperusha mbali.
Kwa nini?’
auliza Yehova wa majeshi.
‘Kwa sababu nyumba yangu ni magofu,
huku kila mmoja wenu
akikimbia huku na huku
ili kuitunza nyumba yake mwenyewe.
Kwa hiyo
mbingu zilizo juu yenu
zikazuia umande wake,
na dunia
ikazuia mazao yake.
Nami niliendelea
kuuita ukame uje duniani,
milimani,
kwenye nafaka,
kwenye divai mpya,
kwenye mafuta,
kwenye mimea inayoota ardhini,
juu ya wanadamu
na mifugo,
na juu ya kazi yote
ya mikono yenu.’”
Yehova analinganisha
matokeo ya ubinafsi wa Wayahudi
na kibarua anayeweka
mshahara wake katika
mfuko uliojaa mashimo.
Kwa kuwa Wayahudi
wanaipuuza nyumba ya Yehova,
anawanyima baraka zake.
Wanapata matokeo machache
kutokana na jitihada zao,
na kwa kweli hawana furaha.
Watu fulani wanajaribu kujifariji kwa
kupamba nyumba zao.
Lakini vitu vya kimwili,
haviwezi kutosheleza mahitaji ya kiroho.
Je, tunaona onyo kwetu?
Si vibaya kuwa na vitu vizuri vya kimwili.
Lakini vitu vya kimwili
haviwezi kutuletea shangwe ya
kweli na ya kudumu,
hasa ikiwa tunapuuza
kazi ya Yehova ili kuvipata.
Kumbuka somo tunalopata
kwenye Zaburi 127:1:
“Yehova asipoijenga nyumba,
wale wanaoijenga
wanafanya kazi ngumu ya bure.”
Kwa upande mwingine,
‘tunapoutafuta kwanza
Ufalme na uadilifu wake’,
Yehova atatuandalia kile tunachohitaji
na atafanya hivyo
kwa wakati unaofaa kabisa.
Methali 10:22 inatuambia hivi:
“Baraka ya Yehova
ndiyo inayomtajirisha mtu,
naye haichanganyi na maumivu.”
Je, hekalu hilo litakalojengwa upya
litakuwa na utukufu kama
ule wa hekalu la Sulemani?
Kupitia Hagai,
Yehova anahakikisha
kwamba utukufu wa nyumba hiyo
utakuwa mkubwa
kuliko ule wa Sulemani.
Tuendelee kusoma Hagai 2:3 hadi 9.
Ni nani aliyebaki
miongoni mwenu ambaye
aliiona nyumba hii
katika utukufu wake wa mwanzoni?
Sasa mnaionaje?
Je, hamwoni kwamba ni duni
ikilinganishwa na ilivyokuwa?
Lakini sasa jipe moyo Zerubabeli,
asema Yehova,
jipe moyo Yoshua
mwana wa Yehosadaki,
kuhani mkuu.
Nanyi watu wote wa nchi,
jipeni moyo,
asema Yehova,
‘na mfanye kazi.
Kwa maana niko pamoja nanyi,
asema Yehova wa majeshi.
Kumbukeni ahadi
niliyowapa mlipotoka Misri,
na roho yangu bado
imo miongoni mwenu.
Msiogope.
Kwa maana Yehova wa majeshi
anasema hivi:
Kwa mara nyingine tena
baada ya muda mfupi
nitatikisa mbingu na dunia
na bahari na nchi kavu.
Nami nitayatikisa mataifa yote,
na vitu vyenye thamani vya mataifa yote
vitaingia katika nyumba hii;
nami nitaijaza nyumba hii utukufu,
asema Yehova wa majeshi.
Fedha ni yangu,
na dhahabu ni yangu,
asema Yehova wa majeshi.
Utukufu wa wakati ujao wa nyumba hii
utakuwa mkubwa zaidi kuliko
ule wa mwanzoni,
asema Yehova wa majeshi.
Na mahali hapa nitawapa amani,
asema Yehova wa majeshi.
Muumba na mmiliki wa ulimwengu mzima
anapotangaza kusudi lake,
ni nani au ni nini kinachoweza kumzuia?
Hakuna kinachoweza kumzuia!
Ujumbe wa Yehova
uko wazi kabisa.
Lakini bado Wayahudi waliorudi
walihitaji kutiwa moyo zaidi.
Yehova anamtuma malaika wake
aende kwa nabii mwingine,
Zekaria.
Tafadhali fungua Zekaria 1:12 hadi 16,
na tusome maneno yenye
kutia moyo ambayo malaika
aliliambia taifa la Israeli.
Zekaria 1:12 hadi 16.
Basi malaika wa Yehova akauliza:
Ee Yehova wa majeshi,
utaendelea hadi lini kukataa
kuwaonyesha rehema
wakaaji wa Yerusalemu
na wa majiji ya Yuda,
ambao umewakasirikia kwa miaka hii 70?
Yehova akamjibu kwa maneno ya fadhili
na yenye kufariji malaika huyo
aliyekuwa akizungumza nami.
Kisha malaika huyo aliyekuwa
akizungumza nami akaniambia:
Tangaza hivi kwa sauti,
“Yehova wa majeshi anasema hivi:
‘Nina bidii kwa ajili ya Yerusalemu
na Sayuni,
bidii nyingi.
Kwa hasira kali nimeyakasirikia
mataifa yanayostarehe,
kwa sababu niliwakasirikia
kidogo watu wangu,
lakini yalizidisha msiba wao.’
Basi Yehova anasema hivi:
‘Nitarudi Yerusalemu kwa rehema,
na nyumba yangu mwenyewe
itajengwa humo,’
asema Yehova wa majeshi,
‘na kamba ya kupimia
itanyooshwa juu ya Yerusalemu.’”
Ili kukazia jinsi Yehova
atakavyowalinda watu wake,
malaika huyo anaendelea
kusema hivi kwenye sura ya 2,
mstari wa 7 hadi 9:
Njoo, Ee Sayuni!
Kimbia, wewe unayekaa na
binti ya Babiloni.
Kwa maana hivi ndivyo
anavyosema Yehova wa majeshi,
ambaye baada ya kutukuzwa
amenituma kwa mataifa
yaliyokuwa yakiwapora ninyi:
“Yeyote anayewagusa ninyi
anaigusa mboni ya jicho langu.
Kwa maana sasa
nitaupunga mkono wangu dhidi yao,
nao watakuwa nyara
kwa watumwa wao wenyewe.”
Na hakika mtajua kwamba
Yehova wa majeshi amenituma.
Ungemruhusu mtu akuguse
kwenye mboni ya jicho?
Bila shaka la!
Yehova pia hatawaruhusu
wapinzani wa Waisraeli wawadhuru.
Kwenye Zekaria 3:1 na 2,
malaika huyo anafunua
adui mwenye nguvu zaidi ambaye
ndiye chanzo cha upinzani.
Naye akanionyesha
kuhani mkuu Yoshua akiwa amesimama
mbele ya malaika wa Yehova,
na Shetani alikuwa amesimama
kwenye mkono wa kulia wa Yoshua
ili kumpinga.
Kisha malaika wa
Yehova akamwambia Shetani:
Yehova na akukemee,
ewe Shetani, naam,
Yehova,
ambaye amechagua Yerusalemu,
na akukemee!
Je, mtu huyu si gogo
lililochomolewa motoni?
Je, hayo yote yalikusudiwa
kuwafanya Waisraeli wajiamini
kwa sababu ya uwezo wao wenyewe?
La hasha!
Walihitaji kukumbuka
kwamba hawawezi
kutimiza jambo lolote
bila msaada wa Yehova.
Sikiliza maneno yafuatayo ya
malaika huyo kwenye Zekaria sura ya 4,
mstari wa 6 na 7:
Hili ndilo neno la Yehova
kwa Zerubabeli:
“‘Si kwa jeshi,
wala si kwa nguvu,
bali kwa roho yangu,’
asema Yehova wa majeshi.
Wewe ni nani,
Ee mlima mkubwa?
Mbele ya Zerubabeli
utakuwa nchi tambarare.
Naye ataleta nje
jiwe la juu kabisa la hekalu
huku watu wakishangilia:
‘Ni zuri ajabu!
Ni zuri ajabu!’”
Wakiwa wamechochewa
na maneno ya Yehova
kupitia manabii wake wawili,
Wayahudu wanaacha
kuwa na shaka na wanaanza
kujenga tena hekalu.
Kama ilivyotarijiwa,
maadui ambao ni majirani wa Israeli,
wakiongozwa na Tatenai
na Shethar-bozenai,
wanajaribu kuvuruga kazi hiyo.
Tusome tena Ezra,
sura ya 5, mstari wa 3 hadi 5:
Wakati huo
Tatenai gavana wa
eneo lililo Ng’ambo ya Mto
na Shethar-bozenai
na wenzao wakaja na kuwauliza:
Ni nani aliyewaagiza
mjenge nyumba hii
na kukamilisha nguzo hizi?
Pia, wakawauliza:
Wanaume wanaojenga
jengo hili ni akina nani?
Lakini Mungu alikuwa
pamoja na wazee wa Wayahudi,
nao hawangeweza kuwazuia
kabla ya kumwandikia Dario
na kupata barua rasmi
kuhusu jambo hilo kutoka kwake
Hilo ni somo lingine kwetu leo:
Tunapoendelea kufanya kazi ya Yehova
kwa ujasiri licha ya upinzani,
Yehova anabariki jitihada zetu
na kutuwezesha kuendelea kumtumikia.
Lakini, kwa sasa
wanapaswa kuendelea na
kazi yao ya kujenga hekalu
licha ya marufuku.
Mfalme aliyepiga marufuku kazi yao
aliuawa baada ya
kutawala kwa miezi saba tu.
Kwa hiyo, Tatenai na wenzake
wanashughulika na mfalme mpya,
Dario wa kwanza.
Wanapowashutumu Wayahudi,
wanajaribu kutumia
maneno ya Zerubabeli
dhidi yake mwenyewe,
kutia ndani maneno aliyosema
kwamba Mfalme Koreshi
ndiye aliyetoa agizo la
kujenga upya hekalu.
Wanamwomba Mfalme Dario
afanye utafiti
ili kuhakikisha
ukweli wa maneno hayo.
Dario anaagiza uchunguzi ufanywe.
Mfalme Dario atafanya uamuzi gani?
Je, imani ya Wayahudi iliyochochewa
na iliyoimarishwa itawaletea shangwe?
Au italeta matatizo zaidi?
Dario aligundua kwamba
Koreshi alitoa agizo la
kujenga upya hekalu hilo.
Tunasoma jibu kali alilolitoa
kwenye Ezra 6:6 hadi 12.
Basi, Tatenai
gavana wa eneo lililo Ng’ambo ya Mto,
Shethar-bozenai,
na wenzenu,
magavana wadogo wa
eneo lililo Ng’ambo ya Mto
msikaribie mahali hapo.
Msiingilie kazi ya nyumba hiyo ya Mungu.
Gavana wa Wayahudi
na wazee wa Wayahudi
watajenga upya nyumba hiyo ya Mungu
mahali ilipokuwa zamani.
Pia, ninatoa agizo
kuhusu jambo mnalopaswa
kuwafanyia wazee hao wa Wayahudi
kwa ajili ya kujenga upya
nyumba hiyo ya Mungu:
Gharama zao zote
zitalipwa bila kuchelewa
kutoka katika hazina ya mfalme,
kodi inayokusanywa
katika eneo lililo Ng’ambo ya Mto,
ili ujenzi uendelee bila kukatizwa.
Na chochote kinachohitajiwa
ng’ombe dume wachanga
pamoja na kondoo dume
na wanakondoo kwa ajili ya dhabihu
za kuteketezwa
kwa Mungu wa mbinguni,
ngano,
chumvi,
divai,
na mafuta,
kama watakavyosema
makuhani walio Yerusalemu
waendelee kupewa vitu hivyo
siku baada ya siku
bila kukosa,
ili waendelee kutoa matoleo
yanayompendeza Mungu wa mbinguni
na kumwombea mfalme na wanawe
wawe na maisha marefu.
Pia nimetoa agizo kwamba
yeyote atakayevunja amri hii,
nguzo itang’olewa katika nyumba yake
naye atatundikwa juu ya nguzo hiyo,
na nyumba yake itafanywa
kuwa choo cha umma
kwa sababu ya kosa hilo.
Na Mungu aliyefanya jina lake likae huko
na ampindue mfalme yeyote
na watu watakaonyoosha mkono
ili kukiuka agizo hili
na kuiharibu nyumba ya Mungu,
iliyo Yerusalemu.
Mimi, Dario,
ninatoa agizo hili.
Nalo litekelezwe bila kukawia.
Baada ya kupokea amri ya mfalme,
Tatenai na wenzake wanasalimu amri.
Hawakupaswa tu kuacha kuzuia
kazi ya ujenzi wa hekalu,
bali pia wanapaswa
kulipia gharama za ujenzi!
Wayahudi waaminifu wanashangilia sana
kupata uamuzi huo.
Mwaka 515 K. W. K.,
wanazindua nyumba ya Mungu
kwa shangwe,
ona maneno tunayosoma kwenye
mstari wa 22:
Pia, wakasherehekea
kwa shangwe Sherehe ya
Mikate Isiyo na Chachu kwa siku saba,
kwa maana Yehova aliwafanya washangilie
na alikuwa ameugeuza moyo wa
mfalme wa Ashuru
ili awatendee mema,
hivi kwamba akawaunga
mkono katika kazi
ya nyumba ya Mungu wa kweli,
Mungu wa Israeli.
Leo, maofisa wenye hekima
na wanaofuata haki wanapotumia
mamlaka yao kutusaidia,
tunashukuru sana.
Lakini tunashukuru zaidi
kwamba Yehova anaelekeza mambo.
Kama Methali 21:1 inavyosema:
“Moyo wa mfalme ni kama
vijito vya maji mkononi mwa Yehova.
Yeye huuelekeza mahali
popote anapopenda.”
Kwa hiyo,
hatuweki tegemeo letu katika mtawala
au shirika lolote la ulimwengu huu.
Hakuna yeyote kati yao anayeweza
kutuletea wokovu wa kudumu.
Kabla ya mwisho wa
mfumo huu wa Shetani,
mataifa yote yatawashambulia
watu wa Yehova.
Lakini mataifa yatapatwa
na hali mbaya kuliko
ile iliyompata Tatenai.
Tunajifunza masomo gani
kutokana na sehemu hizo za Ezra,
Hagai,
na Zekaria?
Kwanza,
Yehova anabariki jitihada zetu za
kuendelea kufanya kazi yake
licha ya changamoto,
lakini hawaruhusu
wapinzani waizuie kazi yetu.
Pili, tunapotanguliza
kazi ya Yehova mbele ya vitu vya kimwili,
anatupatia shangwe ya kweli.
Yesu ametukabidhi kazi gani leo?
Katika maneno yake ya mwisho
kwa wafuasi wake,
alisema hivi waziwazi:
“Basi,
nendeni
mkafanye wanafunzi kutoka
kwa watu wa mataifa yote.”
Kupitia mambo tunayofikiria na kutenda,
Je, tunaonyesha kwamba huo ndiyo
mgawo muhimu zaidi kwetu?
Hagai alitabiri kwamba siku moja,
hekalu la Yehova
lingekuwa na utukufu mkubwa
kuliko lile lililojengwa na Sulemani.
Unabii huo unatimizwa leo.
Yehova anatumia
kazi yetu ya kuhubiri
kuyatikisa mataifa.
Mamilioni ya “vitu vyenye thamani,
yaani,
waabudu wapya,
wanakuja kwake.
Wanamiminika kwa shangwe
katika hekalu kubwa la kiroho
mpango wa Yehova wa kumwabudu
kwa msingi wa dhabihu
ya fidia ya Yesu Kristo.
Huu si wakati wa kukazia fikira
“nyumba zilizopambwa kwa mbao”
au katika utendaji mwingine
usio wa lazima.
Hivi karibuni sana,
katika siku ambayo hatutarajii,
ulimwengu wa Shetani utakoma,
nasi tutaingia katika
ulimwengu mpya wa Yehova.
Kwa hiyo, hata Shetani
ajaribu kufanya nini kutuvunja moyo,
na kutukengeusha,
na tusimruhusu atunyang’anye
shangwe yetu ya kumtumikia Yehova!
Na tuendelee kutembea pamoja na Yehova
mpaka tutakapoingia
katika ulimwengu wake mpya wenye amani,
ambapo tutamtumikia milele kwa shangwe.
Zerubabeli,
Yeshua,
Hagai,
na Zekaria
wamefanya mengi kuwasaidia Waisraeli
kupata tena kibali cha Yehova.
Katika mwaka wa 468 K. W. K.,
Ezra mwenyewe alifika Yerusalemu
kuunga mkono ibada ya kweli.
Lakini bado taifa linahitaji mwongozo zaidi.
Kwa hiyo,
Yehova anamtuma kiongozi mwingine jasiri.
Wakati wa siku mbili zifuatazo
za kusanyiko hili,
tutajifunza kumhusu mwanamume
huyo mwaminifu na mwenye nguvu
Nehemia.