JW subtitle extractor

Utangulizi wa Waroma

Video Other languages Share text Share link Show times

‎Utangulizi wa kitabu cha Waroma.
‎Kitabu cha Waroma
‎kimewekwa kwanza katika orodha ya barua 21
‎za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.
‎Mtume Paulo aliandika barua 14 kati ya hizo,
‎kutia ndani Waroma.
‎Huenda Paulo alianza safari yake ya tatu ya umishonari
‎katika mwaka wa 52 W.K.
‎Alipokuwa Korintho katika mwaka wa 56 W.K.,
‎Paulo aliwaandikia Wakristo waliokuwa Roma,
‎jiji ambalo kufikia wakati huo hakuwa amelitembelea.
‎Barua kwa Waroma ina sura 16.
‎Katika sura ya 1,
‎Paulo anaelezea tamaa yake ya kuwatembelea Wakristo wanaoishi Roma
‎ili waweze kutiana moyo.
‎Pia anaeleza kwamba mwenendo wa ulimwengu usiompendeza Mungu
‎hauwezi kutetewa kwa sababu sifa za Mungu zisizoonekana
‎zinaonekana kupitia kazi zake za uumbaji.
‎Je, ulijua?
‎Paulo alimtumia Tertio kuandika barua hii.
‎Huenda dada mwaminifu anayeitwa Fibi
‎ndiye aliyeipeleka barua hii kule Roma
‎au aliandamana na yule aliyeipeleka.
‎Katika sura ya 2,
‎Paulo anakazia kwamba Mungu hana ubaguzi.
‎Wayahudi na Watu wa Mataifa watahukumiwa
‎kwa kutegemea kiwango kilekile.
‎Katika sura ya 3 na ya 4,
‎Paulo anaeleza kwamba Yehova
‎anawatangaza Wayahudi na Wagiriki kuwa waadilifu kwa msingi wa imani,
‎na anatumia mfano wa Abrahamu kuonyesha jambo hilo.
‎Abrahamu aliishi kabla ya Musa kupewa Sheria
‎na kabla ya Yesu kudhabihu uhai wake.
‎Hata hivyo, Mungu alimwona Abrahamu kuwa mwadilifu
‎kwa sababu ya imani yake ya pekee.
‎Katika sura ya 5 na ya 6,
‎Paulo anaeleza jinsi Adamu alivyotenda dhambi dhidi ya Mungu
‎na kwa sababu hiyo wanadamu wote wamerithi dhambi na kifo.
‎Kitulizo kinapatikana tu kwa kuwa na imani katika Yesu
‎na kifo chake cha kidhabihu.
‎Katika sura ya 7 na ya 8,
‎Paulo anaonyesha jinsi Sheria ya Musa ilivyofunua dhambi ni nini
‎na kwa nini Wakristo hawako chini ya Sheria hiyo.
‎Katika sura ya 9 na ya 10,
‎Paulo anaeleza kwamba wale wanaoonyesha imani
‎wanaweza kuwa watoto wa kiroho wa Mungu,
‎haidhuru walizaliwa katika taifa gani.
‎Katika sura ya 11,
‎Paulo anatoa mfano kuhusu mzeituni.
‎Wayahudi waliomkataa Masihi
‎wanalinganishwa na matawi yaliyokatwa.
‎Badala yao matawi kutoka kwenye mzeituni wa mwituni,
‎yanayowakilisha Wakristo wasio Wayahudi,
‎yalipandikizwa.
‎Ili kuwa sehemu ya mti huo,
‎kila mmoja anapaswa kuendelea kuwa mnyenyekevu
‎na kumwamini Yesu.
‎Katika sura ya 12 na ya 13,
‎Paulo anawasihi Wakristo wafanye amani na watu wote,
‎wapendane,
‎na waheshimu mamlaka za serikali.
‎Katika sura ya 14 na ya 15,
‎Wakristo wanashauriwa waache kuhukumiana
‎badala yake wawategemeze walio dhaifu.
‎Katika sura ya 16,
‎Paulo anamalizia kwa maneno yenye kutia moyo
‎na kutoa salamu changamfu za kibinafsi
‎akiwataja watu 26 kwa jina.
‎Unaposoma barua kwa Waroma
‎ona jinsi Mungu anavyoshughulika bila ubaguzi na watu wote,
‎jinsi Wakristo wanavyopaswa kufanya amani na wengine,
‎na jinsi uhuru kutoka kwa dhambi na kifo
‎unavyowezekana tu kwa kuwa na imani katika Yesu,
‎Mfalme wa Ufalme wa Mungu.